Wednesday 2 August 2017

Marekani yakana kutaka kuing’oa Korea Kaskazini

Serikali ya Marekani kupitia waziri wa maswala ya kigeni Rex Tillerson, imesema haina dhamira ya kuing’oa madarakani utawala wa Korea Kaskazini, wakati huu ambao kumekuwa na hali ya wasiwasi juu ya mpango wa silaha za nyuklia wa Pyongyang.

 “Sisi siyo maadui” alisema Tillerson na kuongeza kuwa Marekani ilihitaji majadiliano kwa kiasi fulani.

Pamoja na kauli ya waziri huyo, seneta mmoja mwandamizi wa Chama cha Republican amesema rais Trump amelipa uzito suala la kuingia kwenye vita na taifa hilo la Korea Kaskazini, akiamini kuwa hilo ndilo chaguo sahihi.

Yenyewe Korea Kaskazini inadai kuwa jaribio lake la hivi karibuni la kombora la masafa marefu, linaweza kupiga pwani ya Magharibi ya Marekani na sehemu nyingine.

“Hatutafuti mabadiliko ya madaraka, hatutafuti anguko la utawala, sisi siyo maadui zenu, sisi siyo tishio kwenu, lakini mnawasilisha tishio lisilokubalika kwetu na tunapaswa kujibu,” alisema Tillerson akiiambia Korea Kaskazini.

0 comments:

Post a Comment