Thursday 27 July 2017

JPM 'aipa tano' TCU kwa kufungia vyuo

Rais John Magufuli ameipongeza Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kwa kuzuia udahili wa wanafunzi wote wa mwaka kwanza katika vyuo vikuu 19 na kuzuia udahili wa wanafunzi wa kozi 75 katika vyuo vikuu 22 kutokana na dosari zilizobainika wakati wa ukaguzi wa ubora vyuo hivyo uliofanyika Oktoba 2016.

Rais Magufuli ametoa pongezi hizo alipowasili jijini Dar es Salaam leo akitokea mkoani Dodoma ambapo akiwa katika eneo la Tegeta wilaya ya Kinondoni amezungumza na wananchi wa eneo hilo.

“Ndugu zangu nchi hii ilishakuwa kila kitu hewa hewa, tumegundua wafanyakazi hewa zaidi ya 19,500, kulikuwa na mikopo hewa ya wanafunzi, na naipongeza TCU kwa kufungia baadhi ya vyuo kudahili wanafunzi, nafanya yote haya kwa ajili yenu, nataka tuwe na nchi nzuri,” amebainisha rais Magufuli.

 Rais Magufuli ameahidi kuendelea kuchukua hatua mbalimbali za kukabiliana na kero na kuimarisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.“Mimi nitafanya kazi kwa nguvu zangu zote na kwa kumtanguliza Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Watanzania wote hasa wanyonge ambao siku zote walikuwa wakionewa,” amesema rais Magufuli

Baadhi ya juhudi alizozitaja kufanyika tangu aingie madarakani ni pamoja na kuondoa ada kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari, kuongeza mikopo ya wanafunzi wa vyuo vikuu kutoka shilingi bilioni 371 hadi kufikia shilingi bilioni 483, kukabiliana na vitendo vya rushwa na ufisadi na kulinda mali za umma hasa madini.

“Kwenye madini tumeibiwa sana, nchi yetu ni kati ya nchi zinazoongoza kwa kuibiwa, tumeibiwa kwa miaka 18, sasa imetosha,” amesisitiza rais Magufuli.

0 comments:

Post a Comment