Tuesday 16 May 2017

Kijana Marekani afariki baada ya kunywa kafeini nyingi kwa haraka

Davis Cripe
Davis Cripe alikunywa vitaji tatu vya kafeini chini ya masaa mawili
Kijana aliyekuwa buheri wa afya amefariki baada ya kunywa vinywaji vyenye kiwango cha juu sana cha kafeini (dutu inayopatikana katika vinywaji kama vile kahawa).
Davis Allen Cripe alizirai katika shule moja ya sekondari mwezi wa Aprili baada ya kunywa kahawa aina ya 'Latte' kutoka McDonalds pamoja na kinywaji cha Mountain Dew na kuongezea kinywaji chenye sukari nyingi kinachotumiwa kuongeza nguvu mwilini, kwa muda wa chini ya masaa mawili, alisema mpasuaji maiti Gary Watts.
Hakuwa na ugonjwa wowote wa moyo na licha ya kuwa na uzani wa kilogramu 90, hakuwa mnene.
"Hatusemi kuwa alikufa kutokana na kiwango cha kafeni alichokunywa bali ni namna alivyokunywa vinywaji vyote kwa haraka na kisha kubugia hicho kinywaji chenye sukari nyingi kinachotumiwa kuongeza nguvu mwilini," Watts alieleza Reuters.
Kafeinie haingedhaniwa kuwa moja ya chanzo cha kifo chake ikiwa wachunguzi hawangepata habari kuhusu kinywaji alichotumia kabla ya kufa, alisema mpasuaji maiti huyo wa jimbo la Richland.
Shahidi mkuu hakuweza kusema kinywaji cha tatu alichokunywa Davis kilikuwa cha kampuni gani .
"Tunajaribu kutoonekana ni kama tunawashawishi watu kuwachana na kafeini kabisa," Watts alisema. "Tunaamini watu wanapaswa kuwa waangalifu wanakunywa kiwango gani cha kafeni, na ni vipi wanainywa, kama wanavyofanya kwa pombe au sigara."
Baadhi ya vinywaji vinavyotumiwa kuongeza nguvu mwilini
AAP imeonya dhidi ya watoto na vijana kunywa vinywaji vyenye sukari nyingi vinavyotumiwa kuongeza nguvu mwilini
Chuo cha Wataalamu wa Maradhi Marekani (AAP) wameonya dhidi ya watoto na vijana kunywa vinywaji vyenye sukari nyingi vinavyotumiwa kuongeza nguvu mwilini kwani viungo vilivyotumiwa kuvitengeneza havijulikani ni vya kiwango kipi na vina athari gani kwa watoto.
AAP inasema vinywaji hivi vina madhara, ikiwa ni pamoja na mapigo ya moyo yasiyo ya kawaida na mabadiliko ya shinikizo la damu.
Nyingi ya vinywaji hivi vina kafeni ya kiwango sawa na vikombe vitatu vya kahawa na wastani wa vijiko 14 vya sukari.
Huenda Davis alikunywa miligramu 470 za kafeini chini ya masaa mawili, kulingana na takwimu za kutoka kwenye tovuti ya caffeineinformer.com.
Inasema 'latte' ya McDonald ina miligramu 142 ya kafeni, na mililita 570 ya kinywaji cha Mountain Dew na miligramu 90, huku mililita 450 ya kinywaji chenye sukari nyingi kinachotumiwa kuongeza nguvu mwilinii ikiwa na uwezekano wa kuwa na miligramu 240 za kafeini.
Mwaka wa 2015, Mamlaka ya Ulaya ya Usalama wa Chakula Marekani ilisema kunywa zaidi ya miligramu 400 za kafeni kunaweza kusababisha kuongezeka kwa kiwango cha mdundo wa moyo, shinikizo kubwa la damu, mapigo ya moyo, kutetemeka, woga na kukosa usingizi .
Kunywa vikombe vichache vya kahawa na vinywaji vingine vilivyo na kafeni kwa siku ni sawa.
Lakini kunywa kupita kiasi au kunywa nyingi katika kipindi kifupi ni hatari.
Miligramu 400 ya kafeini kwa siku moja inaonekana kuwa salama kwa watu wazima walio sawa kiafya.
Hiyo ni takribani kiasi cha kafeni katika vikombe vinne vya kahawa au makopo 10 ya Coca-Cola.
Vijana na wanawake wajawazito wanashauriwa kunywa chini ya kiwango hiki na watoto wachanga nao hawafai kupewa kafeni.

source:bbc

0 comments:

Post a Comment